Home KITAIFA MWENYEKITI MPYA BODI YA REA AANZA KAZI RASMI NA KUSISITIZA UCHAPAKAZI, UADILIFU

MWENYEKITI MPYA BODI YA REA AANZA KAZI RASMI NA KUSISITIZA UCHAPAKAZI, UADILIFU

Google search engine
Mwenyekiti Mpya wa Bodi ya Nishati Vijijini, Janeth Mbene akizungumza na Wajumbe wa Bodi hiyo pamoja na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Februari 11, 2023 jijini Dar es Salaam.

Na Veronica Simba  – REA

MMWENYEKITI mpya wa Bodi ya Nishati Vijijini, Janeth Mbene ameanza kazi rasmi kwa kukutana na kuzungumza na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ambapo amesisitiza uchapakazi, weledi, uadilifu na ushirikiano katika kazi.

Katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam leo, Februari 11, 2023 na kuhudhuriwa pia na Wajumbe wa Bodi, Mwenyekiti amehamasisha kufanya kazi kwa ufanisi ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa katika kuwasaidia wananchi hususan wa vijijini kupata maendeleo.

“Tujitahidi sana kufanya kazi vizuri, kwa weledi na kwa wakati huku tukisimamia maeneo ambayo tunapaswa kuyasimamia kwa karibu sana hasa wakandarasi wanaotekeleza miradi mbalimbali,” amesisitiza Mwenyekiti.

Akizungumza zaidi, Mbene ameeleza kuwa maendeleo ya kiuchumi yanategemea sana nishati za aina zote, hivyo akatoa hamasa kwa wafanyakazi wa REA kupitia Menejimenti kutumia vizuri rasilimali kidogo zinazopatikana ili tija yake ionekane.

Amesema REA ni Taasisi yenye umuhimu mkubwa kwa Taifa kutokana na mchango wake katika maendeleo hususani ya wananchi wa vijijini. “Na kwa hali hiyo hii kazi tuliyopewa siyo ndogo,” amesisitiza.

Zaidi, Mwenyekiti amewataka wote kuhakikisha wanafanya kazi inayoacha alama na kwa namna hiyo kuzitendea haki nafasi walizopewa kuwatumikia Watanzania.

Akizungumza kwa niaba ya Menejimenti na Wafanyakazi wote wa REA, Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Hassan Saidy amemhakikishia Mwenyekiti ushirikiano na kwamba watatekeleza yote aliyoyaagiza.

Awali, Wajumbe wa Menejimenti walipata fursa ya kujitambulisha kwa Mwenyekiti na kila mmoja kueleza majukumu yanayotekelezwa katika Idara/Kitengo anachosimamia.

Janeth Mbene aliteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, Februari Mosi, 2023 na kutangazwa Februari 3, mwaka huu kushika nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini baada ya Mtangulizi wake kumaliza muda wake.

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy akieleza majukumu ya Wakala hiyo kwa Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Nishati Vijijini, Janeth Mbene (katikati) katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam, Februari 11, 2023.
Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini, wakimsikiliza kwa makini Mwenyekiti mpya wa Bodi hiyo, Janeth Mbene (hayupo pichani) wakati wa kikao baina ya Mwenyekiti na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kilichofanyika jijini Dar es Salaam
Wajumbe wa Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), wakimsikiliza kwa makini Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Nishati Vijijini, Janeth Mbene (hayupo pichani) wakati wa kikao baina ya Mwenyekiti na Menejimenti hiyo kilichofanyika jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy akieleza majukumu ya Wakala hiyo kwa Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Nishati Vijijini, Janeth Mbene (katikati) katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam
Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here