Home KITAIFA Tanzania inatarajia kutundika satelite yake kulinda nchi

Tanzania inatarajia kutundika satelite yake kulinda nchi

Google search engine
Naibu waziri wa habari na teknolojia ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew (wapili kulia) akipokea maelezo kutoka kwa Afisa wa benki ya NMB, Doreen Sawe (kushoto) alipotembelea banda la benki ya NMB katika mkutano mkuu wa mwaka wa wakaguzi wa mifumo ya Mtandao (ISACA) unaofanyika kwa siku nne katika hoteli ya Gran melia Jijini Arusha. Kulia ni Rais wa ISACA Tanzania, Peter Baziwe na watatu kulia ni Katibu wa ISACA Tanzania, Rosevita Majani na wengine ni viongozi wa Chama cha wakaguzi wa mifumo ya kimtandao Tanzania.
 

NA MWANDISHI WETU

-ARUSHA

Arusha.

Katika kuimarisha mifumo ya ulinzi nchini, Tanzania inatarajia kutundika satellite yake ya kwanza angani itakayotumika pia katika kuboresha huduma za mawasiliano.

Hayo yamesemwa jijini Arusha na Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari nchini, Eng. Kundo Mathew wakati akifungua mkutano mkuu wa Mwaka wa wakaguzi wa mifumo ya Mtandao (ISACA) unaofanyika kwa siku nne katika hotel ya Gran Melia.

Alisema kuwa Mradi huo ni mwendelezo wa uboreshaji wa miundo mbinu ya mawasiliano nchini mara baada ya kufanikiwa kujenga mkongo wa Taifa na kuotesha minara 758 ardhini, sasa wanahamia angani ambapo mchakato wa uwekaji satellite unaanza.

Alisema katika utekelezaji wa mradi huo, timu ya wataalamu yenye wadau mbali mbali imeshaundwa itakayokuwa chini ya wizara yake yenye lengo la kufanya utafiti wa mahitaji ya nchi juu ya Satelite hiyo kabla haijawekwa.

“Katika mradi huu wa Satelite hatukurupuki, tunachukua muda kutambua mahitaji yetu inayopendekezwa ya Taifa, na timu imeundwa ya kutafakari matumizi yaliyokusudiwa kama je, itakuwa tu kwa ajili ya kushika doria anga zetu, au kulinda rasilimali zetu kutoka angani au labda pia kufuatilia mipaka ya nchi kidijitali?” alibainisha Mhandisi Mathew.

Alisema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkataba wa Malabo ambao pamoja na mambo mengine,  unahusu ulinzi wa anga za kitaifa na hii ni kutokana na shughuli nyingi za kimtandao kuongezeka ikiwemo upenyezaji wa mawasiliano ya kidijitali. na miamala ya kifedha.

“Kuna maeneo yenye vilima na milima mikubwa ambapo inakuwa vigumu kwa mionzi na nyaya za ‘fiber optic’ kutandazwa, hapa ndipo satelaiti itachukua nafasi ya kueneza mawimbi ya kidijitali, ambayo pia inaweza pia kutumika kwa ajili ya mawasiliano ya jeshi na shughuli nyingine za usalama.

Aidha Eng. Kundo alitumia nafasi hiyo kuwataka wataalamu hao wa ISACA kufanya ufuatiliaji wa mifumo hiyo yote na kukagua kama umezingatia viwango na ubora wa ndani kulingana na mahitaji lakini pia wa kimataifa (ITU) ili kuziba mianya yanayoonekana katika utendaji kazi kwenye taasisi za serikali na binafsi hasa kwa ulinzi wa kinchi.

“Mapinduzi makubwa kwenye sekta ya mawasiliano yanakuja na sisi kama serikali mbali na kujenga mifumo hii tunakwenda kuboresha zaidi sheria,na kanuni za kimtandao ili kulinda taarifa binafsi za watu lakini pia kuwe na usalama wa shughuli zinazofanyika huko ikiwemo miamala ya kifedha lakini pekee yetu hatuwezi bali tunawategemeeni ninyi kufanikisha” Alisema Eng. Kundo

Aidha Mkutano huo wa Mwaka wa 2023 wa Ukaguzi, Hatari na Usalama wa Mtandao wa ISACA umewakutanisha zaidi ya wataalamu mbali mbali 250 kutoka taasisi na makampuni ya serikali na binafsi kupeana uzoefu wa matukio waliyokumbana nayo katika ukaguzi wa mifumo, udhibiti, usalama  wa mtandao na utawala, ili kuchukua tahadhari za mapema katika kukabiliana na hatari.

Akizungumzia mkutano huo mjumbe wa bodi ya ISACA, Halfan Semindu, alisema kuwa mkutano huo mkuu wa mwaka umekutanisha wajumbe kutoka taasisi, makampuni mbali mbali nchini ili kupeana taarifa na walibadilishana uzoefu juu ya kile kinachoendelea duniani kote na kile kinachoweza kuigwa nchini Tanzania, lengo ikiwa kuchukua tahadhari ya maswala ya usalama kimtandao.

“ISACA ni chama iliyoko katika nchi 184 sasa na hapa tuna wawakilishi kutoka nchi nyingi ikiwemo Kenya, Nigeria, Commoro, Djibout ambao tunabadilishana uzoefu wa yale tunayokutana nazo, ujuzi wa ukaguzi wa usalama wa mtandao hii itatusaidia kama nchi kuchukua tahadhari za mapema za kiusalama” alisema.

Kwa upande wake mjumbe wa ISACA kutoka Zanzibar, Kenneth Wakaji alisema kuwa wameanza kutoa mafunzo ya ukaguzi wa mifumo kwa wafanyakazi kutoka taasisi mbali mbali za binafsi na serikali na kuwapa vyeti lengo ikiwa ni kupanua wigo wa wataalamu wengi wa usalama wa mtandao watakaosaidia kazi ya ulinzi wa Taifa.

Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here