Home MICHEZO ‘Vuta Nikuvute’ NMB vs Baraza la Wawakilishi Z’bar

‘Vuta Nikuvute’ NMB vs Baraza la Wawakilishi Z’bar

Google search engine

Afisa Mkuu Wetu wa Wateja Wakubwa na Serikali, Alfred Shao akimkabidhi baadhi ya vifaa vya michezo Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Zubeir Ali Maulid leo katika ofisi za Baraza hilo ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Bonanza la Michezo kati ya Benki ya NMB na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi lililofanyika jijini Zanzibar. 
 

NA MWANDISHI WETU, ZANZIBAR

BONANZA la Kudumisha Mashirikiano baina ya Benki ya NMB na Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), linaunguruma Jumamosi hii ya Juni 10, kwenye Viwanja  vya Mao-Tse-Tung, ambalo litatanguliwa na Matembezi ya Hisani yatakayoanzia Viwanja vya BLW – Chukwani, yakiongozwa na Spika wa Baraza, Mhe. Zubeir Ali Maulid. 

Baada ya matembezi hayo yatakayoanza saa 12 asubuhi, timu za taasisi hizo zitachuana kuwania vikombe mbalimbali vya katika michezo ya mpira wa miguu, kikapu, riadha, kukimbiza kuku, kuvuta kamba na kukimbia na magunia, kisha washindi kuzawadiwa.

Kuelekea bonanza hilo, NMB kupitia Afisa Mkuu wa Wateja Wakubwa na Serikali, Alfred Shao, alimkabidhi Spika Zubeir Maulid msaada wa vifaa vya Michezo, zikiwemo jezi na ‘track-suit,’ ambavyo vilikabidhiwa kwa manahodha wa timu za michezo hiyo wakiongozwa na Nahodha Mkuu, Hamza Hassan Juma, ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais – Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Spika Maulid aliishukuru NMB kwa jinsi inavyojitoa kuunga mkono juhudi za kuleta maendeleo zinazofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), na kuutaja ushirikiano wao na BLW kama uthibitisho wa utayari wao katika kuwahudumia na kuwajali Wazanzibar. 

“Tunawashukuru NMB kwa wazo la kufanya bonanza hili, lakini pia kwa juhudi za kusapoti Baraza na Serikali kwa ujumla katika kuiletea Zanzibar maendeleo. 

“Tunapokea vifaa hivi, na tuko tayari kwa bonanza yatakayoanza na Matembezi ya Hisani kesho, tukiamini timu zetu zitafanya vema. Ahadi yetu (BLW) ni kudumisha ushirikiano na NMB, benki ambayo imekuwa nasi bega kwa bega kwenye masuala mbalimbali, yakiwemo ya kukuza Uchumi wa Vullu,” alisisitiza Spika Maulid. 

Awali, Shao alisema katika kuazimisha miaka 25 ya huduma bora za kifedha nchini, NMB inalitumia bonanza hilo kutoa shukrani kwa jamii, iliyochagiza mafanikio ya benki iliyoanza 1997 ikitambulika kama Benki ya Walalahoi,  hadi sasa inapoongoza Sekta ya Fedha Tanzania. 

“Tunaposherehekea miaka 25, ambako licha ya kampeni endelevu ya upandaji miti milioni moja kwa mwaka huu, tumeona tutumie bonanza hili kurejesha kwa jamii iliyotufikisha hapa. Tunaamini bonanza hili na Wawakilishi hawa wa Wazanzibar, litaakisi dhamira yetu ya kudumisha undugu na ushirikiano baina yetu.

“Tumejiandaa kushinda bonanza hili, huku ahadi yetu kwa SMZ na BLW ni kuendelea kusapoti jitihada za kufanikisha Ustawi wa Wazanzibar na kukuza Uchumi wa Vullu,” alisisitiza Shao, ambaye alisema tayari NMB imeshapanda miti 548,000 kati ya milioni moja waliyopanga kuipanda kote nchini mwaka huu.

Kwa upande wake, Hamza Hassan Juma ambaye ni nahodha wa BLW, aliipongeza NMB kwa vifaa mbalimbali ilivyowakabidhi, huku akiisifu kwa utayari na uharaka wao wa kuisaidia SMZ, ambako ni mara chache sana wameombwa, badala yake wamefanya hivyo mara nyingi bila kuombwa.

Hamza, ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais – Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi, aliiahidi NMB kwamba Wajumbe wa BLW na Wazanzibar, wako tayari kutumia kila fursa zilizopo katika benki hiyo ili kuharakisha ukuaji kiuchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla. 

Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here