Home KITAIFA TANZANIA, COMORO KUANZIASHA TUME YA KUDUMU

TANZANIA, COMORO KUANZIASHA TUME YA KUDUMU

Google search engine

Na MWANDISHI WETU

-BEST MEDIA

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Comoro zimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) wa kuanzisha Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya nchi hizo mbili.

Makubaliano hayo yamesainiwa leo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Stergomena Tax na Waziri wa Mambo ya Nje wa Comoro, Dhoihir Dhoulkamal katika Ubalozi wa Tanzania, Addis Ababa, Ethiopia.

Mara baada ya kusaini kwa mkataba huo wa makubaliano, Dk. Tax alisema kuwa Tanzania na Comoro zina uhusiano wa kihistoria na mataifa hayo yamekuwa yakishirikiana katika maeneno mbalimbali, hivyo kusaini makubaliano hayo kutaziwezesha nchi hizo kufanya kazi kwa ukaribu na ushirikiano zaidi ikiwemo kuanza mchakato wa Mkutano wa Kwanza wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kwa maslahi ya nchi hizi mbili.

“Tanzania na Comoro tumekuwa tukishirikiana katika sekta za biashara na uwekezaji, afya, kijamii, siasa, ulinzi na usalama pamoja na miradi ya kiuchumi hivyo kusaini kwa makubaliano haya kutatuwezesha kufanya kazi kwa ukaribu zaidi,” amesema Dk. Tax

Kwa Upande wake,Dhoulkamal ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kukubali kuanzisha Tume ya Kudumu ya Pamoja na utayari wa Comoro kuendelea kushirikiana na Tanzania kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, hususani diplomasia ya uchumi.

“Tanzania imekuwa rafiki wa Comoro kwa muda mrefu, tunaamini kusainiwa kwa makubaliano haya leo……kutatuwezesha kufungua fursa mpya mbalimbali za kiuchumi kwa maslahi mapana ya mataifa yetu,” alisema Mhe. Dhoulkamal. Aidha, Dk. Tax yupo Addis Ababa nchini Ethiopia kushiriki Mkutano wa 42 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika unaotegemewa kufanyika tarehe 15 – 16 Februari, 2022.

Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here